Sunday, June 13, 2010

IJUE SAYARI

                                                     
Sayari ni (gimba la angani) kubwa linalozunguka jua na kung'aa kutokana na nuru ya jua iliyoakisiwa, tofauti na nyota na jua zinazong'aa pekee.
Jua letu lina sayari nane. Toka mwaka 1930 hadi Agosti 2006 Pluto ilikuwa ikitambulika kama sayari hivyo kufanya idadi ya sayari zinazojulikana kuwa tisa. Hata hivyo chama chenye mamlaka ya masuala ya sayari na nyota, (International Astronomical Union) kimetangaza rasmi kuwa Pluto sio sayari na kuiita sayari kibeti.
Sayari tano za Utaridi, Zuhura, Meriki, Mshtarii na Zohari huonekana kwa macho kama nyota angani. Lakini tangu zamani zilitambuliwa kuwa tofauti kwa sababu hazikai mahali palepale kama nyota ya kawaida bali huhamahama angani. Kutokana na tabia hii zimetazamiwa mara nyingi kuwa na nguvu za pekee au hata kuwa miungu. Unajimu imetumia mwendo wa sayari zinazoonekana kwa macho kama msingi muhimu wa makadirio yao.
Sayari nyingine katika mfumo wa jua zimetambuliwa tangu kutokea kwa falaki ya kisayansi kwa darubini. Hizi ni Uranus na Neptun. Katika lugha ya Kiswahili sayari zinazoonekana kwa macho huwa na majina ya asili ya Kiarabu isipokuwa Zuhura ni sayari lenye jina la Kibantu la Ng'andu pamoja na jina la asili ya Kiarabu. Majina mengine ni ya asili ya Kilatini.
Jumla ya jua, sayari zote pamoja miezi yao, vimondo, nyotamkia na asteroidi inaitwa mfumo wa jua.
Wataalamu wa falaki wamegundua sayari hata nje ya mfumo wa jua letu zinazozunguka nyota mbalimbali. Kutokana na umbali mkubwa na matatizo ya utazamaji hakuna uhakika hadi sasa kama nyota kuwa na sayari ni jambo la kawaida angani au kama sayari ni chache tu.

No comments:

Post a Comment